Uswahilishaji wa Tanzania kama Hatua ya Ukombozi Kamili: Dhana na Mikakati ya Kimatendo

21
Uk. wa 1 kati ya 21 Uswahilishaji wa Tanzania kama Hatua ya Ukombozi Kamili: Dhana na Mikakati ya Kimatendo Athumani S. Ponera Mhadhiri, Idara ya Kiswahili Chuo Kikuu cha Dodoma Simu: +255 767 95 97 84 Baruapepe: [email protected] Ikisiri Lugha ya Kiswahili ni mhimili mkuu wa michakato mbalimbali ya kupatikana kwa uhuru hapa Tanzania. Ni matarajio ya viongozi na wananchi wote kuwa baada ya kuwa huru maendeleo yangefululiza katika nyanja mbalimbali za maisha yao. Hata hivyo, hatua ya kimaendeleo iliyofikiwa haiendani na uhalisi wa matarajio. Kutofikiwa huko kumekuwa kukizua manung’uniko na malalamiko katika nyanja mbalimbali. Malalamiko haya ni ithibati ya kutokuwapo kwa ukombozi kamili. Miongoni mwa sababu za kutofikiwa kwa matarajio ya Watanzania kimaendeleo ni tandabelua iliyopo kuhusu matumizi ya lugha. Katika uga wa elimu, mathalani, kumekuwapo malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali kuhusu kuchujuka kwake kunakoendelea kutokea. Shabaha ya makala hii ni kutalii hali hii kwa jicho mahususi, huku ikirejelea tafiti, maoni na mapendekezo yaliyowahi kutolewa na viongozi, watafiti, na wanaisimu mbalimbali. Tiba inayoibuliwa humu kuhusu namna ya kuukomboa mfumo wa elimu wa Tanzania ni Uswahilishaji, yaani, hali ya kukifanya Kiswahili kitamalaki katika nyanja zote muhimu za maisha (k.v. elimu, uchumi, sayansi, tiba) kwa watu wanaotumia lugha ya Kiswahili kama lugha yao ya kwanza au ya pili. Kutamalaki huko, hatimaye, kutakifanya Kiswahili kiwe bidhaa na zana ya kiukombozi. Makala imeegemea katika elimu kwa kuamini kuwa iwapo elimu itaswahilishwa, ni wazi kuwa ni rahisi kwa vipengele vingine vyote vya maisha ya Waswahili kuswahilishwa pia. Dhana hii ya Uswahilishaji imejadiliwa huku ikijiegemeza katika maswali yafuatayo: a) Uswahilishaji ni nini? b) Vikwazo vya Tanzania Kuswahilishwa ni vipi? c) Ucheleweshwaji wa Uswahilishaji una athari gani kwa kizazi cha sasa na baadaye? d) Kizazi cha sasa kifanye nini ili Kuiswahilisha Tanzania? 1 Istilahi muhimu: Uswahilishaji, ukombozi kamili, mikakati ya kimatendo. 1 Makala hii ilinenepeshwa na maoni ya washiriki wa mijadala ya semina za kitaaluma za Vyuo Vikuu viwili, Chuo Kikuu cha Waislamu Morogoro (iliwasilishwa na kujadiliwa Januari 28, 2013) na Chuo Kikuu cha Dodoma (iliwasilishwa na kujadiliwa Mei 8, 2013).

Transcript of Uswahilishaji wa Tanzania kama Hatua ya Ukombozi Kamili: Dhana na Mikakati ya Kimatendo

Uk. wa 1 kati ya 21

Uswahilishaji wa Tanzania kama Hatua ya Ukombozi Kamili: Dhana na Mikakati ya Kimatendo

Athumani S. Ponera

Mhadhiri, Idara ya Kiswahili

Chuo Kikuu cha Dodoma

Simu: +255 767 95 97 84

Baruapepe: [email protected]

Ikisiri

Lugha ya Kiswahili ni mhimili mkuu wa michakato mbalimbali ya kupatikana kwa uhuru

hapa Tanzania. Ni matarajio ya viongozi na wananchi wote kuwa baada ya kuwa huru

maendeleo yangefululiza katika nyanja mbalimbali za maisha yao. Hata hivyo, hatua ya

kimaendeleo iliyofikiwa haiendani na uhalisi wa matarajio. Kutofikiwa huko kumekuwa

kukizua manung’uniko na malalamiko katika nyanja mbalimbali. Malalamiko haya ni ithibati

ya kutokuwapo kwa ukombozi kamili. Miongoni mwa sababu za kutofikiwa kwa matarajio ya

Watanzania kimaendeleo ni tandabelua iliyopo kuhusu matumizi ya lugha. Katika uga wa

elimu, mathalani, kumekuwapo malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali kuhusu kuchujuka

kwake kunakoendelea kutokea. Shabaha ya makala hii ni kutalii hali hii kwa jicho mahususi,

huku ikirejelea tafiti, maoni na mapendekezo yaliyowahi kutolewa na viongozi, watafiti, na

wanaisimu mbalimbali. Tiba inayoibuliwa humu kuhusu namna ya kuukomboa mfumo wa

elimu wa Tanzania ni Uswahilishaji, yaani, hali ya kukifanya Kiswahili kitamalaki katika

nyanja zote muhimu za maisha (k.v. elimu, uchumi, sayansi, tiba) kwa watu wanaotumia

lugha ya Kiswahili kama lugha yao ya kwanza au ya pili. Kutamalaki huko, hatimaye,

kutakifanya Kiswahili kiwe bidhaa na zana ya kiukombozi. Makala imeegemea katika elimu

kwa kuamini kuwa iwapo elimu itaswahilishwa, ni wazi kuwa ni rahisi kwa vipengele vingine

vyote vya maisha ya Waswahili kuswahilishwa pia. Dhana hii ya Uswahilishaji imejadiliwa

huku ikijiegemeza katika maswali yafuatayo: a) Uswahilishaji ni nini? b) Vikwazo vya

Tanzania Kuswahilishwa ni vipi? c) Ucheleweshwaji wa Uswahilishaji una athari gani kwa

kizazi cha sasa na baadaye? d) Kizazi cha sasa kifanye nini ili Kuiswahilisha Tanzania?1

Istilahi muhimu: Uswahilishaji, ukombozi kamili, mikakati ya kimatendo.

1 Makala hii ilinenepeshwa na maoni ya washiriki wa mijadala ya semina za kitaaluma za Vyuo Vikuu viwili, Chuo Kikuu

cha Waislamu Morogoro (iliwasilishwa na kujadiliwa Januari 28, 2013) na Chuo Kikuu cha Dodoma (iliwasilishwa na

kujadiliwa Mei 8, 2013).

Uk. wa 2 kati ya 21

1.0 Utangulizi

Lugha ya Kiswahili imekuwa nembo muhimu sana ya kulitambulisha eneo la Afrika Mashariki

duniani kote. Kiswahili, kama lugha ya mawasiliano hutumiwa na watu wa nchi za ukanda wote wa

Afrika Mashariki. Baadhi ya nchi hizo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, na Jamhuri ya

Kidemokrasia ya Kongo. Kwa kigezo cha jumla (cha kiisimujamii), kati ya nchi hizo, Tanzania

inajichomoza kama nchi ya Kiswahili (na kwa hivyo, ni nchi ya Waswahili). Hii ni kutokana na

mazingira ya kiisimujamii ambapo Kiswahili kinatumika katika nchi ya Tanzania kwa shughuli zote.

Nchini Tanzania, Kiswahili ni lugha rasmi; pia ni lugha ya taifa. Kwa jumla, Kiswahili ni zaidi ya lugha

kwa Watanzania; Kiswahili ndiyo maisha yenyewe! Hii ni kwa sababu, hutumiwa na kila mtu katika kila

tukio, kila muktadha, kila mahali, na kila wakati. Shughuli mbalimbali nchini Tanzania kama vile siasa,

utamaduni, utawala, utendaji, elimu, michezo, burudani, na hata mazungumzo hutumia Kiswahili kwa

namna ya moja kwa moja au kwa uficho. Shughuli hizi zinatumia Kiswahili bila kujali kama zinafanywa

na watu wa kada, mazingira wala kiwango fulani cha elimu. Hali hii ilikuwepo toka nyakati za kabla ya

uhuru. Licha ya kutamalaki huko kwa lugha ya Kiswahili katika maisha ya Watanzania, bado eneo nyeti

la elimu linasuasua kutokana na matumizi hafifu ya lugha hii. Wataalam wengi wameshafanya tafiti

mbalimbali kuhusu mgogoro huu wa matumizi ya Kiswahili katika elimu nchini Tanzania.

Baadhi ya tafiti hizo ni ule uliofanywa na Mlama na Matteru (1978) kuhusu „Haja ya Kutumia

Kiswahili Kufundishia katika Elimu ya Juu‟. Hawa, katika ripoti yao, walibainisha jinsi lugha ya

Kiingereza inavyoathiri ujifunzaji katika ngazi za kuanzia sekondari na kuendelea. Na wakapendekeza

kuwa Kiswahili kitumike badala ya Kiingereza; na kwa kufanya hivyo, kitakuzwa na kuwa lugha ya

kitaalamu. Pia, walipendekeza kuwa mbinu za ufundishaji wa lugha za Kiingereza ziboreshwe. Utafiti

mwingine ulifanywa mwaka 1984 na Waingereza, Ciper na Dodd; chini ya ufadhili wao. Hawa

walijikita katika kuchunguza ujuzi wa wanafunzi katika lugha ya Kiingereza. Majawabu ya utafiti wao

yakaonesha kuwa kiwango cha wanafunzi wa shule mbalimbali za sekondari katika lugha ya Kiingereza

Uk. wa 3 kati ya 21

ni kidogo sana. Baada ya utafiti huu, ndipo mnamo mwaka 1986 serikali ya Uingereza ikaanzisha mradi

maalum wa kuimarisha Kiingereza katika shule za sekondari.

Tafiti nyingine zilizofanyika miaka ya hiyo ya 1980 na mwanzoni mwa miaka ya 1990 kuhusu

matumizi ya lugha katika elimu nchini Tanzania ni ule wa 1986 wa Campbell na Qorro; pamoja na ule

wa 1991 uliofanywa na Rubagumya. Campbell na Qorro waliutafiti uwezo wa wanafunzi wa shule za

sekondari katika kuelewa vitabu vilivyoandikwa kwa lugha ya Kiingereza. Walibaini na kubainisha

kuwa asilimia 95 ya wanafunzi siyo tu hawawezi kuelewa, bali pia hawawezi kusoma vitabu hivyo.

Rubagumya (1991), kwa upande wake, alichunguza matumizi ya lugha za Kiswahili na Kiingereza

katika shule za sekondari. Alionyesha kwamba lugha ya Kiingereza inatumika kwa sababu tu ya

kulazimishwa na sera. Matokeo ya kulazimishwa huko ni kwamba sehemu kubwa ya mafundisho

hutolewa na walimu kwa kutumia Kiswahili. Pia, mijadala mingi ya ujifunzaji ifanywayo na wanafunzi

hufanywa kwa Kiswahili. Zaidi, utafiti wa Rubagumya ulibaini kuwa siyo wanafunzi tu, bali, hata

walimu wana uwezo mdogo wa kutumia lugha ya Kiingereza katika ufundishaji. Kwa ujumla, matokeo

ya tafiti hizo zote yameonyesha kuwa jamii ya Watanzania inataabishwa na matumizi ya Kiingereza

katika uga wa elimu.

Nje ya uga huo wa elimu pia kuna matatizo na mataabiko makubwa kuhusu matumizi ya lugha

hizi mbili, yaani Kiswahili na Kiingereza. Hapa ninakusudia nyuga kama vile za utawala, sheria, na

utabibu. Miongozo ya kiserikali inatambua na kuafiki kuwa Kiingereza kitumike kwa mawasiliano

katika nyuga hizo na nyinginezo. Katika baadhi yazo, Kiingereza kinatumika nusunusu (kwa

kuchanganya na Kiswahili) na katika nyinginezo kinatumika, au niseme, kinatakiwa kitumike kwa

asilimia mia. Mathalani, katika mazingira ya elimu ya juu, lugha ya Kiingereza inatakiwa itumike siyo

tu kama lugha ya kufundishia na kujifunzia, bali pia mawasiliano mengine yote. Hata hivyo, uhalisi

unaonyesha kuwa bado Kiswahili ndiyo lugha inayotamalaki katika kuendesha shughuli mbalimbali za

asasi za elimu ya juu kama vile vikao, mikutano, na mijadala. Kwa upande wa mazingira ya kitabibu,

Uk. wa 4 kati ya 21

Kiingereza kinatumika nusunusu. Matabibu huitumia kuwasiliana wao kwa wao (katika hatua

mbalimbali za kutibu—kutoka kwa daktari, kwenda kwa m-maabara, kurudi kwa daktari, na kwenda

kwa mfamasia). Mzunguko huu haumhusu kabisa mgonjwa (ambaye ndiye anaandikiwa nyaraka hizo;

na kwamba, ndiye apaswaye kuzirejelea katika ufuatiliaji wa matibabu yake katika tukio la ugonjwa huo

au kwa siku zitakazofuatia). Mifano hii miwili inatosha kutuleta kwenye hoja muhimu kadhaa. Mosi,

nchi haina utaratibu unaoeleweka na madhubuti kuhusu matumizi ya lugha. Pili, ukosefu huo wa

utaratibu maalum unasababisha madhara mengi kwa jamii. Miongoni mwa madhara hayo ni yale

yaliyotajwa katika ripoti za watafiti waliodondolewa hapo juu.

Katika kujaribu kujibu baadhi ya malalamiko na maoni ya wananchi, wanaisimu, wanataaluma

pamoja na watafiti; wanasiasa au watawala wamewahi kuonyesha juhudi kadhaa. Katika juhudi hizo,

kumewahi kutolewa nyaraka, kuundwa kwa tume kadhaa pamoja na kutolewa kwa miongozo na

matamko kuhusu kuanza kutumia Kiswahili kufundishia elimu zetu zote. Juhudi ya kwanza ilitolewa

mwaka 1969. Hii ilihusu waraka wa wizara iliyokuwa inahusika na masuala ya elimu. Waraka huo

ulitumwa kwa wakuu wa sekondari nchini kote wakielezwa kuwa Kiswahili kingeanza kutumika

kufundishia masomo ya sekondari. Matumizi yenyewe yangefanywa kwa awamu tatu na ndani ya miaka

miaka mitatu (kuanzia mwaka 1969 hadi 1971); kwamba, mwaka 1969 matumizi ya Kiswahili

yangeanza kufundishia somo la siasa. Kisha, mwaka 1970 lingefuatia somo la sayansi kimu; na mpango

ungekamilika mwaka 1971 kwa masomo mengine yaliyosalia. Ninaliita wazo hili juhudi kwa kuwa

angalau tunathamini kuwako kwake kinadharia. Hata hivyo, utekelezaji wake haukufanikiwa hata

kuanza!

Miaka kumi baadaye, wizara hiyohiyo ikafufua wazo lake hili kwa kutangaza kuwa “…siku

moja Kiswahili kitafanywa lugha ya kufundishia” (Mdee, 2007). Tangazo hili likakitaka Chuo Kikuu

cha Dar es Salaam kianze maandalizi ya kiutekelezaji (kuandaa vitabu na nyaraka nyinginezo za

kufundishia). Kabla utekelezaji wa tangazo hili haujaanza, Rais akaunda tume ya elimu. Mapendekezo

Uk. wa 5 kati ya 21

ya tume hii yakafufua hamu ya Waswahili wa Tanzania kuhusu kujikomboa kielimu kwa kuitumia lugha

yao wenyewe katika kufikiri na kuunda mawazo mapya. Tume ilipendekeza kuwa Kiswahili kianze

kutumiwa kufundishia katika elimu ya sekondari kuanzia Januari 1985. Na kianze kutumiwa katika

ngazi ya Chuo Kikuu kuanzia mwaka 1992 (yaani ambao wangeanza nacho mwaka 1985 wangeendelea

nacho hadi Chuo Kikuu). Wazo hili lililotokana na kazi iliyotumia kodi za Watanzania nalo lilipotea

hewani kama moshi wa sigara!

Mwaka 1986 wazo hili la kutumiwa kwa Kiswahili katika elimu ya sekondari lilipigiwa tena

mbiu. Safari hii mbiu ilitoka vinywani mwa jopo la wanaisimu. Hawa nao, kama walivyopendekeza

wengine, kwa msisitizo sana walishauri kuondokana na fikra mgando za kung‟ang‟ania kutumia

Kiingereza katika elimu; badala yake Kiswahili kitumike na Kiingereza kifundishwe kama somo la

lazima katika ngazi zote za elimu. Kwa mara nyingine, mawazo mazuri ya wanataaluma hao yakaishia

kufunikwa na mavumbi katika mashubaka!

Miaka kumi baadaye, yaani mwaka 1996 nchi ikaingia tena katika mjadala, tena safari ukiwa

mzito (pengine ni kwa sababu ya mpanuko wa vyombo vya habari nchini pamoja na imani ya watu

kuwa Rais mpya wa wakati huo — Rais Mkapa alikuwa na vionjo vya kupenda lugha). Wazo

lilifufuliwa na Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) ambao walikwenda ikulu kumpongeza Ndugu

Rais kwa kuchaguliwa kwake. Ndani ya salamu hizo za pongezi wakamwomba aruhusu Kiswahili kipate

hadhi yake ya kutumiwa kwa asilimia 100 katika ufundishaji na ujifunzaji wa ngazi zote za elimu.

Jawabu la Ndugu Rais katika kutatua mvutano wa mawazo ya watu waliogawanyika katika pande mbili

(waliopendelea Kiingereza kiendelee kutumiwa na waliopendelea Kiswahili kianze kutumiwa) lilitaka

kuhusishwa kwa wananchi katika maamuzi haya. Hivyo, ilitakiwa uanzishwe utaratibu wa jinsi ya

kuwahusisha wananchi katika jambo hili adhimu. Kwa bahati mbaya, wazo hili zuri la Rais Mkapa

halikuonekana tena kimatendo!

Uk. wa 6 kati ya 21

Awamu ya nne ya utawala wa Tanzania ilianza kwa nuru ya aina yake kwa wadau wa masuala

ya lugha kufuatia kauli ya Rais wa awamu hii, Ndugu Jakaya Mrisho Kikwete katika hotuba yake ya

mwanzo kwa taifa (hotuba ya Disemba 2005) iliyogusia kuuhuisha uzalendo kwa taifa letu. Mwangaza

huo wa furaha ya Waswahili wa Tanzania ulitokana na kuamini kuwa uzalendo huo, pamoja na mambo

mengine, ungehuishwa sana kwa kuheshimu, kuthamini, na kutukuza utamaduni wetu ambapo lugha ya

Kiswahili ni miongoni mwa vielelezo vyake. Huu, kama auitavyo Samala (2003), ni uzalendo wa

kiutamaduni; uzalendo uhusishao lugha, maadili ya taifa pamoja na shauku ya kisanaa. Na kwamba,

Waswahili waliendelea kutumaini kuwa, miongoni mwa matendo ya kuonyesha heshima, thamani, na

utukufu wa lugha ya Kiswahili, kwa ngazi ya kimakuzi iliyofikia kwa sasa ni kuiruhusu itumike rasmi

katika ngazi zote za elimu. Ni takribani miaka nane sasa ndoto hii ya Waswahili bado haijaingia katika

uhalisi!

Kufifishwa kwa maoni hayo ya wataalamu, wanaisimu na wananchi wa kawaida pamoja na

matamko na miongozo ya watawala kuhusu utaratibu mbovu wa kutumia lugha kumeendelea kuiweka

Tanzania katika hali mbaya sana kielimu na kijamii. Wananchi wameendelea kuyumba na

kunung‟unika. Hali ya matumizi ya lugha za Kiswahili na Kiingereza katika miktadha rasmi nchini

Tanzania ni ya kusikitisha sana. Wananchi wengi wana maarifa shinda kuhusu lugha hizi mbili.

Watanzania hawana uhuru kamili wa kutumia Kiswahili katika miktadha rasmi kama vile ya kisheria na

ya kitabibu. Maendeleo yanatokea kwa kusuasua katika nyanja mbalimbali hapa nchini. Lawama na

manung‟uniko yanasikika kutoka kila kona ya nchi kuhusu utaratibu wa matumizi ya lugha. Utaratibu

huo ndiyo unatoa mazao ya kielimu ambayo yanalalamikiwa. Wanafunzi wanalalamika! Walimu

wanalalamika! Wahadhiri wanalalamika! Viongozi wa mashirika mbalimbali wanalalamika! Ajabu zaidi

ni kwamba wahusika wa asasi zihusikazo na uratibu wa masomo na utahini nao wanalalamika! Chanzo

kikuu cha malalamiko hayo ni kulazimishwa kwa matumizi ya lugha ya Kiingereza kuanzia katika elimu

Uk. wa 7 kati ya 21

ya sekondari hadi elimu ya juu. Wanafunzi wanahitimu wakiwa na maarifa nusunusu; hawana uwezo wa

kutosha wa kuleta tija katika maendeleo ya taifa.

Je, nani amsaidie mwenzake kutuliza malalamiko yake? Ni kwa nini maoni ya wananchi,

wataalamu na wanaisimu yanapuuzwa bila kupatiwa majibu yenye kukata kiu? Ni taifa gani liwezalo

kupata ustawi bila kuhusisha fikra za wataalamu wake wa sekta mbalimbali? Ni nini kinakwaza

utekelezaji wa maoni na mapendekezo ya kitaalamu kuhusu suala hili? Ni nani anaridhia kuwapo kwa

manung‟uniko na malalaniko haya? Mataabiko haya yana tija ipi kwa taifa? Ni kweli taifa limefikia

ukomo wake wa kujikwamua kuhusu utaratibu wa matumizi ya lugha kulingana na vigezo faafu vya

kiisimujamii? Makala hii inajaribu kutoa suluhu ya kuondokana na mkwamo huu wa kijamii kwa

kutambulisha matumizi na utekelezaji wa dhana ya Uswahilishaji wa Tanzania.

2.0 Dhana ya Uswahilishaji

Katika makala hii Uswahilishaji unachukuliwa kuwa ni hali ya kuifanya lugha ya Kiswahili

itamalaki na itumike katika nyanja zote muhimu za maisha kama vile elimu, uchumi, sayansi, teknolojia,

utabibu, utawala, na sheria kwa watu wanaotumia lugha ya Kiswahili kama lugha yao ya kwanza au ya

pili (na kwa hiyo, wana umilisi mkubwa wa lugha ya Kiswahili). Hivyo, uswahilishaji unalenga

kikifanya Kiswahili kiwe bidhaa na zana yenye tija kwa Waswahili! Jambo hili ni la kisera, hivyo

linahitaji mipango na mikakati madhubuti ili kuhakikisha kuwa lugha ya Kiswahili inaenea na

kujitokeza bayana katika kila kipengele cha maisha ya Mswahili wa Tanzania. Kupitia dhana ya

Uswahilishaji, Kiswahili kitajitokeza dhahiri katika vipengele mbalimbali vya mawasiliano kama vile

mazungumzo (hili lina unafuu hata sasa), maelezo na maelekezo ya bidhaa, maelezo na maelekezo

huduma, pamoja na nyaraka. Pia, kitajitokeza bayana katika taaluma mbalimbali. Dhana ya

Uswahilishaji hailengi kuzifuta lugha nyinginezo (za makabila wala za kimataifa), bali inalenga

kuichomoza zaidi lugha ya Kiswahili ili kuipa upekee lugha yenyewe na Tanzania kwa ujumla. Hivyo,

dira ya sera hii ya Uswahilishaji yapaswa kutamka bayana kuwa itokeapo mazingira yoyote ya

Uk. wa 8 kati ya 21

kimawasiliano ambayo yatahitaji matumizi ya lugha zaidi ya moja basi Kiswahili kinatakiwa kijitokeze

kwanza na kisha kifuatiwe na lugha hiyo(zo) nyinginezo.

Tanzania, kama ilivyokwisha kudokezwa katika usuli wa makala hii, ni nchi ambayo Kiswahili

ndiyo nembo yake kuu. Uhuru, amani, umoja na mshikamano uliopo katika nchi hii haviwezi kamwe

kutenganishwa na lugha ya Kiswahili. Hata hivyo, mdhihiriko wa nembo hiyo una nguvu zaidi

kinadharia ikilinganishwa na nguvu ya kimatendo. Zaidi ya hilo, mdhihiriko wenyewe una nguvu zaidi

nje ya mipaka ya Tanzania kuliko ndani ya Tanzania. Mbali na Tanzania kujulikana sana na mataifa

mengi ya Afrika na ulimwenguni kwa ujumla kama nchi inayolelewa na kuongozwa na Kiswahili, hali

iko tofauti kabisa ndani ya nchi. Mathalani, ni vigumu sana kwa mgeni yeyote atokaye nje ya nchi ya

Tanzania kuonja ladha ya Kiswahili baada tu ya kutua sehemu yoyote ya Tanzania. Hii ni kwa vile,

sehemu kubwa ya maandishi mbalimbali kama vile matangazo ya biashara, na maelekezo yaliyopo

mitaani, barabarani na katika vyombo vya habari yako katika lugha ya Kiingereza. Vilevile, nembo za

bidhaa mbalimbali zipo katika lugha Kiingereza. Katika nchi ya Tanzania, si ajabu kumkuta mtu

anatumia neno au jina la Kiingereza katika kutambulisha au kutangaza bidhaa au eneo lake la biashara

ilhali hajui hata sababu wala maana halisi ya jina au neno lenyewe. Matangazo kama vile „Ponera

Restaurant’, „Stella Saloon’, au „Rashid Barbering Shop’ ni mengi sana nchini Tanzania. Haya ni

majina yanayobuniwa na wamiliki wa ofisi husika. Ubunaji na matumizi ya majina yenyewe, kwa

kawaida, huwa hauzingatii utashi wa kiisimu, bali mazoea tu. Kadhalika, kuna huduma nyingi zitokazo

katika asasi za kiserikali au zisizo za kiserikali pamoja na makampuni binafsi na kwenda kwa wananchi

wa kawaida huku zikitumia lugha ya Kiingereza. Mathalani, baadhi ya nyaraka za kiserikali, maelekezo

ya sehemu kubwa ya dawa, vipengele mbalimbali vya huduma za simu (kama vile maelezo ya simu

zenyewe, na kadi za muda wa maongezi) hupatikana katika lugha ya Kiingereza.

Hali hii, licha ya kuchukuliwa kuwa ni ya kawaida mbele ya macho ya Watanzania, ni sehemu

kubwa sana ya udhaifu wa nchi katika kupangilia matumizi ya lugha katika mazingira ya uwingi-lugha

kama ya Tanzania. Ni ajabu sana katika nchi ambayo Kiswahili kinatumiwa na zaidi ya asilimia 97,

Uk. wa 9 kati ya 21

kuona maelekezo na matangazo ya biashara yanatumia lugha ya Kiingereza kwa zaidi ya asilimia 83

(chanzo: utafiti mdogo wa kuchunguza matumizi ya lugha katika nembo, maelekezo na matangazo ya

biashara katika mitaa na vyombo vya habari). Jamii nyingi hapa ulimwenguni hujitahidi kutafuta namna

yoyote ya kujipa upekee katika mambo chanya. Hufanya hivyo kwa kutumia vipengele mbalimbali

kulingana na makubaliano na mahitaji yao. Lugha ni miongoni mwa vipengele hivyo. Hata hivyo, ni

nchi chache sana ulimwenguni huweza kufikia maafikiano katika matumizi ya lugha. Hii ni kutokana na

ukweli kwamba jamii au nchi nyingi zimo katika hali ya uwingi-lugha. Chambilecho Buliba na

Wenzake (2006:108) kuwa “Fikra inayotumika kupanga lugha lazima ioane na matakwa na matarajio ya

jamii inayopangiwa lugha”. Hivyo, Tanzania, ikiwa mojawapo ya nchi chache zenye kiwango kidogo

cha mgongano wa lugha (kwamba angalau Kiswahili kinajulikana, kinatumiwa na kukubaliwa na

sehemu kubwa ya wananchi wake), iko katika nafasi nzuri sana ya kujitengenezea upekee na tija kubwa

kupitia lugha ya Kiswahili. Kinyume chake, licha ya wananchi kutangaza matakwa na matarajio yao

kwa lugha ya Kiswahili, bado „fikra sahihi‟ kuhusu jinsi ya kuitumia kutupatia tija zaidi hazijapatikana.

Hivyo basi, kwa kuwa mpaka sasa tayari wananchi wa kawaida, wanaisimu, na wanataaluma wa

taaluma nyinginezo (nje ya isimu) wameonesha kukihitaji Kiswahili katika nyanja muhimu za maisha

yao kama vile elimu, sayansi na tiba, ni vema basi tukaingia kimatendo katika kuiswahilisha nchi yetu.

3.0 Kwa nini Tanzania Haijaswahilishwa Hadi Leo?

Nimekwishagusia hapo juu kuhusu juhudi kadhaa zilizokwisha kufanywa katika kukifanya

Kiswahili, mbali ya kuwa lugha ya mawasiliano kama ilivyo hivi sasa, kiwe lugha ya kitaaluma, pia iwe

taaluma. Hoja na ufafanuzi wa kutosha umetolewa. Swali muhimu hapa ni kwamba tatizo ni nini? Nani

anakwaza kutokea kwa jambo hili? Jambo lililo bayana kuhusu maswali haya ni kwamba hakuna

majawabu bayana yaliyosikika kupinga matumizi ya Kiswahili kuanzia elimu ya sekondari na

kuendelea. Kauli pekee iliyowahi kusikika kuhusu kutotumiwa kwa Kiswahili katika elimu ya juu ni ile

ya Rais wa kwanza, Ndugu Mwalimu Nyerere. Mdee (2006:194) amedai kuwa Mwalimu Nyerere,

Uk. wa 10 kati ya 21

akihutubia wadau wa UKUTA, alisema bayana kuwa Kiswahili kisitumike kufundishia elimu ya juu

kwa hofu ya kuiua lugha ya Kiingereza ambayo aliiita kuwa ni „Kiswahili cha dunia‟. Pengine kauli hii

ndiyo iliyowapofua sana viongozi wa serikali, vyama vya siasa, mashirika, makampuni, asasi za elimu

na taasisi mbalimbali. Kwa maoni yangu, upofu huu ndiyo unawafanya wasiwe tayari hata kupokea

mapendekezo ya wataalamu wala kuruhusu mijadala kuhusu suala hili. Ninaamini kuwa rai hii ya

Mwalimu Nyerere ilitolewa katika miktadha tofauti sana na iliyopo hivi sasa. Miktadha ninayoikusudia

hapa ni ya kiwakati, makuzi ya uelewa, mwamko wa wananchi, kiasi cha uhitaji, pamoja na mtagusano

wa kijamii. Kwa wakati wake, Mwalimu aliweza kueleweka, au niseme, hao wachache waliokuwa na

fursa ya kupata taarifa walimwelewa. Hivi sasa, jamii ya Watanzania ama inahitaji majawabu na

ufafanuzi wa kutowezekana kwa Uswahilishaji wa Tanzania au utendekeji wa dhana ya Uswahilishaji.

Kwa jumla, kwa maoni yangu, hali hii imekwazwa na makundi makubwa mawili ambayo ni

wananchi wa kawaida pamoja na wananchi waliopata fursa ya kuwa wasomi/wanataaluma, wanasiasa na

viongozi. Wananchi wa kawaida, kwa upande wake, limechangia kwa kiasi kidogo kutokana na tabia za

upole na uanakondoo. Kauli hii ninaitoa kutokana na ukweli kuwa viongozi na wanasiasa huwekwa

madarakani na wanachi ili wawatumikie kwa yale yanayopaswa kukubaliwa na wote. Sasa, kwa suala

hili la kutotumiwa kwa Kiswahili katika elimu ya sekondari na ya juu, Watanzania watu wazima

hatuwezi kukwepa kabisa shutuma za watoto wetu na vizazi vijavyo kwa adha mbalimbali zitokeazo

kwalo. Matakwa tunayo, matarajio tunayo, malengo tunayo, uwezo pia tunao; kwa nini tukubali kuishi

pasipo kupatiwa majawabu ya matakwa na matarajio yetu kuhusu matumizi ya Kiswahili kwa asilimia

100 katika maisha yetu hapa nchini?

Upande mwingine, tena huu ni mkubwa zaidi, wapo wasomi wa taaluma mbalimbali, wanasiasa

na watawala. Hawa, kwa maoni yangu, wamechangia kutoswahilishwa kwa Tanzania kwa kwa kiasi

kikubwa. Kuna sababu kadhaa zinazonisukuma kuwatwisha wadau wa kundi hili uzito mkubwa wa hali

hii: Mosi, hawa ndiyo wenye upeo mkubwa wa kuona na kutafakari kuhusu utendekaji wa masuala

Uk. wa 11 kati ya 21

mbalimbali ya kijamii. Kwa hili, pengine wametafakari ila wanapata kigugumizi kisicho na msingi

kudhihirisha athari za tafakuri zao. Pili, kundi hili ndilo lenye watu waliopewa dhamana ya kuliongoza

taifa kuelekea kwenye ustawi wa kimaisha. Hata kama hatua za kiustawi tulizozifikia katika nyanja

mbalimbali ni nzuri, kwa maoni yangu, zingekuwa nzuri zaidi kama nchi hii ingesikiliza matakwa na

matarajio ya wananchi wake kwa lugha ya Kiswahili. Tatu, katika kundi hili ndimo kuna Watanzania

wanaoshangaza sana kwa kuwa wapo katika nafasi nzuri ya kuboresha sera na mipango-lugha katika

elimu, lakini huishia kuungana na walalamikaji! Mathalani, humu ndimo kuna wanaisimu, wahadhiri na

viongozi wa Vyuo Vikuu ambao hawaishi kulalamikia uwezo duni wa wanafunzi na wahitimu wao

katika taaluma pamoja na umilisi duni wa lugha ya Kiingereza. Je, wanafanya nini ili kuliondoa tatizo

hili? Yatosha tu kuishia kufanya utafiti na kutoa matokeo na kisha kuridhia yaishie kugubikwa na vumbi

huko mashubakani? Kwa ujumla, wadau wa kundi hili, kwa makusudi au bila kukusudia, ndiyo kiini cha

mataabiko mengi wayapatayo Watanzania kuhusu kutokuwapo kwa sera, mipango wala mikakati

madhubuti ya lugha ya Kiswahili.

Mbali na mgawanyo huo wa jinsi jamii ilivyoshiriki kukwamisha Uswahilishaji wa Tanzania,

sababu za jumla za tatizo hili zipo katika makundi makubwa mawili, yaani sababu za ndani na za nje.

Sababu za ndani ni zile zitolewazo na wapinzani wa kuswahilishwa kwa Tanzania waliomo ndani ya

nchi (ambapo nyingi hutolewa na kundi lenye wasomi, wanasiasa na viongozi). Sababu za nje ni zile

zinazotokana na kani na sera za mataifa ya nje.

3.1 Sababu za ndani

kundi hili linahusisha sababu zifuatazo:

a) Kuhusu gharama za Uswahilishaji

Kwamba, mchakato wa kuiswahilisha nchi unahitaji gharama kubwa. Washadidiaji wake wanadai kuwa

ni gharama sana kutafsiri maarifa mengi ambayo yapo katika lugha ya Kiingereza kwenda Kiswahili.

Uk. wa 12 kati ya 21

Hapa wanarejelea vitabu vya kiada na ziada vya kuanzia kidato cha kwanza hadi ngazi ya Chuo Kikuu.

Majawabu ya hoja hii yamekwishatolewa vizuri na watetezi wengi waliowahi kuandika kuhusu jambo

hili. Kwa ufupi, washadidiaji wa pingamizi hili wanasahau kuwa kupanga ni kuchagua! Kwamba, iwapo

tutalimakinikia jambo hili, tunahitaji wastani wa bilioni 60 tu kulifanya litokee kimatendo — izingatiwe

hapa kuwa hizi ni pesa zenye uwezo wa kujenga uwanja mmoja tu wa mpira wa miguu kama ule wa

Taifa ulioko Temeke! Zaidi ya hilo, si lazima pesa hizo zitolewe katika bajeti ya mwaka mmoja. Je,

katika maisha yetu hapa Tanzania, kuna mambo mangapi yasiyo na tija kwa umma yanayoteketeza kiasi

cha pesa kama au zaidi ya hicho? Jawabu jema zaidi kuhusu hoja hii ni kwamba tayari juhudi za

kuandaa nyenzo za kufundishia na kujifunzia kama vile vitabu na kamusi zilikwishaanza na zimefikia

katika hatua nzuri. Tayari kuna vitabu vya kufundishia masomo ya kemia, fizikia na bayolojia

vimekwisha kuandaliwa. Baadhi yavyo, kwa mfano, kitabu cha kemia kiitwacho Furahia Kemia

(kilichoandaliwa na kuchapishwa na Taasisi ya Taaluma za Kiswahili) kipo madukani na kinagombewa

sana na walimu na wanafunzi wa somo hilo. Kitabu hiki kimeandikwa kwa lugha zote mbili, yaani

Kiingereza na Kiswahili kwa namna ya tafsiri-mkabala (ukurasa mmoja umeandikwa kwa Kiingereza na

ukurasa unaokabiliana nao yametafsiriwa maarifa hayo). Vilevile, tayari kuna kamusi kadha

zilizokwishaandikwa na tayari zinatumika. Kwa mfano, kuna Kamusi ya Sheria, Kamusi ya Tiba na

Kamusi ya Bayolojia, Kemia na Fizikia. Bila shaka, kwa hoja hizi, madai ya wapinzani yamebakia kuwa

chapwa. Kupanga ni kuchagua! Tuchague kuiswahilisha Tanzania, tupange!

b) Kuhusu kutokujitosheleza kwa lugha ya Kiswahili kimsamiati na istilahi

Hoja hii nayo inashadidiwa sana na wapingaji wa Uswahilishaji. Madai yao yanajikita katika kushindwa

kwa Kiswahili kupata msamiati wa dhana mbalimbali hususan za sayansi na teknolojia. Pia,

wanadhihaki utohoaji na ukopaji wa istilahi kadhaa kama vile „kisoma mbali‟, „kompyuta‟, n.k. Pia

wabezaji hawa huenda mbali zaidi hadi kukifungamanisha Kiswahili na lugha ya Kiarabu, hivyo, kudai

kuwa Kiswahili siyo lugha kamili kwa sababu ya madai kuwa takribani theluthi mbili ya msamiati wake

Uk. wa 13 kati ya 21

una vionjo vya lugha ya Kiarabu. Hawa nao wamepatiwa majawabu ya kutosha sana na watetezi

walionitangulia. Wanasahau kuwa utohoaji na ukopaji wa msamiati na istilahi ni kaida ya lugha yoyote

(ithibati nzuri ni jinsi ambavyo tunakuta msamiati na istilahi nyingi za Kilatini, Kiyunani au Kifaransa

katika lugha ya Kiingereza ambayo inapapatikiwa). Wanasahau kuwa kisu hupata makali kadri

kinavyotumiwa; na kwamba, Kiswahili kitapata msamiati na istilahi zake katika kila kona kadri jamii

itakavyokuwa inaitumia. Makali hayo yatakuwa yanaongezeka kadri jamii hiyo itakavyokuwa inakua na

kuvumbua vitu mbalimbali na kuvitumia katika maisha yao. Kupanga ni kuchagua. Tuchague

kuiswahilisha Tanzania ili Kiswahili kipate makali zaidi ya kimsamiati, kimuundo, kisemantiki, na

kihadhi.

c) Kuhusu madai kuwa Kiingereza ni lugha ya kitaaluma, kisayansi na ki-ajira

Hoja hii imefanikiwa sana kusambazwa akilini mwa Watanzania. Ithibati ya kutamalaki kwake yaweza

kutazamwa kupitia mhamo wa kifikra unaotokea kwa kasi kuhusu usomeshaji. Wazazi wengi wenye

uwezo wa kiuchumi hufikiria kuwasomesha watoto wao (hususan kwa ngazi ya chekechea na elimu ya

msingi) katika shule zinazotumia lugha ya Kiingereza kama lugha ya mawasiliano na ya kufundishia.

Bila hata kufikiria kuhusu kiasi cha maarifa watakachokipata huko, wazazi wanaamini kuwa watoto wao

watapata „ulimi mwepesi‟ katika lugha ya Kiingereza. Na hatimaye, kuajiriwa katika sehemu nzuri. Kwa

jumla, hawa wanaamini kuwa kujua Kiingereza ndiyo kuelimika. Wanasahau kuwa kama Kiingereza

ndiyo elimu, basi kusingekuwa na ulazima wa kuwa na shule katika nchi ambazo Kiingereza ni lugha

yao ya awali ikiwemo Uingereza yenyewe!

d) Woga wa kizandiki wa wasomi na watawala

Uzandiki hapa umetumika kumaanisha hali ya kuaminisha watu waamini kitu au hali isiyokuwepo; ni

upotoshaji au unafiki. Viongozi wengi na watawala, kwa wazi na kwa ufiche, wameendelea

kuwaaminisha watu kuwa iwapo Kiswahili kitatumika kufundishia sekondari na elimu ya juu, hadhi ya

Uk. wa 14 kati ya 21

elimu itashuka. Hoja hii inaungana kiasi na hoja ya hapo juu kwamba Kiingereza ni lugha ya kitaaluma.

Bali tofauti hapa ni woga unaoshindiliwa kuhusu dhana ya kushuka kwa hadhi ya elimu yetu iwapo

itatolewa kwa Kiswahili. Hoja yangu hapa inalenga kuwakumbusha wapinzani wa Uswahilishaji kuwa

pamoja na hicho Kiingereza kutumiwa hadi sasa, bado hali ya umilisi wake iko chini sana. Hivyo, hoja

hapa iwe kuungana na mapendekezo ya wanazuoni na watafiti kuhusu uboreshaji wa ufundishaji wa

lugha ya Kiingereza. Hili halina ulazima wa kuunganishwa na utumiwaji katika kufundishia (kwa

sababu tayari limekwishashindwa).

e) Kuhusu kushindwa kwa Kiswahili katika elimu ya msingi

Hili ni bezo maarufu kuwa hakuna haja ya kukitumia Kiswahili kufundishia ngazi za juu za elimu kwa

kuwa hata katika ngazi hii ya elimu ya msingi ambayo inakitumia kufundishia na kujifunzia, bado hali

ya ufaulu wa mitihani ni hafifu sana. Hoja hii ya kipropaganda ni dhaifu sana ikimakinikiwa kwa jicho

la kiutendaji. Majawabu ya hoja hii ni haya: Kwanza, hakuna mwanasaikolojia au mwanazuoni yeyote

aliyewahi kusema kuwa ni lazima darasa lote lifaulu mtihani. Zaidi ya hilo, kiwango cha ufanisi wa

wahitimu wa elimu ya msingi hakiwezi kutenganishwa na mfumo mbovu wa kuwatafuta na kuwaandaa

walimu wa wanafunzi hao! Wanafunzi hao hufundishwa na walimu walioathirika na mfumo wa elimu

ya kukaririshwa. Baya zaidi, upatikanaji wa walimu na maandalizi yao, kama asemavyo Kamugisha

(2012), ni wa bahati nasibu. Kwamba, walimu wengi wa Tanzania ni wale waliofaulu kwa kupata daraja

la tatu na la nne. Ni ajabu sana kutumaini mavuno mema kwa mfumo hafifu kama huu wa upataji na

maandalizi ya walimu wa wanafunzi wetu. Jibu jingine lipo kwenye ukweli kuwa kuna tofauti kubwa

sana ya ufaulu wa somo la Kiingereza na masomo mengine yatumiayo Kiswahili. Ufaulu wa somo la

Kiingereza ni wa kiwango cha chini sana ukilinganishwa na ule wa masomo mengine wanayotahiniwa

wanafunzi wanaohitimu elimu ya msingi (Sikombe, 2010).

f) Kutokuwa na sera ya lugha

Uk. wa 15 kati ya 21

Hili ni janga la nchi nyingi za bara la Afrika! Nyingi zimerithi sera na mipango-lugha iliyoachwa na

wakoloni wake. Mathalani, Tanzania mpaka sasa haina sera yake ya lugha, bali tunaendesha masuala ya

lugha kupitia Sera ya Utamaduni ya mwaka 1997. Pamoja na ukweli kuwa lugha ni kijenzi kimojawapo

cha utamaduni, ifahamike hapa kuwa, lugha ndiyo roho ya kuwapo kwa ustawi wa jamii yoyote ile.

Hivyo, kwa mtazamo wangu, kukosekana kwa sera ya lugha inayojitegemea ndiko kumetuleta hapa

tulipo. Kwa kuambatishwa katika Sera ya Utamaduni, matamko yahusuyo lugha yamekosa nguvu ya

kujulikana. Naamini wakati umefika wa kuwa na sera madhubuti ya lugha, na dhana ya Uswahilishaji

iwe ni miongoni mwa mihimili itakayoishikilia sera hiyo.

3.2 Sababu za Nje

Sababu za nje zinahusu kani na mipango ya mataifa ya nje katika kuhakikisha kuwa lugha zao

zinaendelea kuenea na kutumika katika „mataifa madogo‟. Ili kuhakikisha hili linatimia, huweka sera na

mipango kadhaa ili kuyalaghai mataifa haya. Hufanya hivyo huku jicho lao wakilielekeza katika

manufaa ya kiuchumi walengayo kuyapata. Kwa lengo hili, ndipo tunapoona mataifa hayo yakianzisha

mashirika ya lugha zao ili yawe mawakala wa ukuzaji na uenezaji wa lugha hizo. Sera pamoja na

mipango yao hiyo hupata nguvu sana punde kuzukapo vuguvugu la mijadala ya Watanzania kuamshana

kutumia Kiswahili kufundishia katika ngazi zote za elimu. Mathalani, katika mwanzoni mwa miaka ya

1990 kulizuka Operesheni ya kufufua ufundishaji wa Kiingereza inayofadhiliwa na Shirika la

Maendeleo la Uingereza. Ikumbukwe kuwa katika wakati huu nchi ilikuwa katika mjadala na hamu ya

kutaka kuona utekelezaji wa mapendekezo ya ile Tume ya Rais (ya kuanza kutumia Kiswahili kwa

kidato cha kwanza mwaka 1985 na Chuo Kikuu mwaka 1992) pamoja na mjadala wa wanaisimu wa

mwaka 1986. Kwa maoni yangu, hali hii ndiyo iliwasukuma Waingereza kuhuisha mpango wao wa

kufufua Kiingereza ili kufifisha juhudi za Waswahili na hivyo kulifikia lengo lao. Kwa hakika,

nionavyo, ulaghai kama huu ukijumlishwa na vitisho kutoka kwa mataifa haya „makubwa‟ ni sababu

tosha ya kuwasukuma viongozi wetu kupuuza maoni na matakwa ya wanataaluma na wananchi kwa

Uk. wa 16 kati ya 21

jumla. Na hivyo, kuendeleza kasumba ya mataifa ya Afrika ya kuzoea kuishi kikasuku katika masuala

mbalimbali. Wito wangu hapa ni kwa wahusika kujiuliza: Iwapo hayo „mataifa makubwa‟

yanayodhaniwa kuwa lugha zao zina nguvu hayajaridhika na ueneaji wa lugha zao, iweje sisi Waswahili

tuendelee kuzishabikia lugha zao bila kuweka mipango madhubuti ya kuiendeleza lugha yetu? Zaidi ya

swali hilo, napenda kukumbusha hapa kuhusu uhusiano uliopo baina ya ushabiki huu tuufanyao kwenye

lugha ya Kiingereza na utumwa. Chambilecho Gandhi (1965) wakati anajenga hoja ya Wahindi kutumia

Kihindi katika nyanja zote za maisha yao:

… mtumwa hupenda kuiga tabia na mbinu za bwana wake kama vile mavazi, lugha n.k.

Taratibu hupenda tabia za bwana wake na kutupilia mbali mambo yake… Kiingereza

hakiwezi kuwa kuwa lugha yetu ya taifa wala ya kufundishia. Tumezidumaza lugha zetu

kwa kutumia Kiingereza. Tumewapa mzigo mkubwa wanafunzi wetu. Huu utumwa wa

lugha ya kigeni umewanyima mamilioni ya wananchi wetu kupata maarifa mengi muhimu

kwa miaka mingi… [Gadhi (1965:8) kama alivyonukuliwa na Mdee (2007:192-193)].

Maneno haya ya Gandhi yanajitosheleza sana, wala hayahitaji ziada yoyote ili kuleta uelewa na

ushawishi kuhusu hoja hii ya kuiswahilisha Tanzania. Hima, tuiswahilishe Tanzania ili kuachana na

utumwa huu! Katika sehemu ifuatayo nitaeleza hatua tuwezazo kuzifuata ili kuifikia dhana ya

Uswahilishaji kimatendo.

4.0 Mchakato wa Uswahilishaji

Utekelezaji wa dhana ya Uswahilishaji itafikiwa kimatendo iwapo mambo yafuatayo yatazingatiwa:

a) Kutoa tamko la kikatiba kuwa lugha ya Kiswahili ni lugha ya taifa na lugha rasmi ambayo

lazima itumike kwa uhuru na ufasaha katika shughuli na vipengele vyote vya umma nchini

Tanzania. Na kwamba, yatokeapo mazingira yoyote ya kimawasiliano ambayo yatahitaji

matumizi ya lugha zaidi ya moja basi Kiswahili kinatakiwa kijitokeze kwanza na kisha kifuatiwe

na lugha hiyo nyingine;

b) Kuchambua na kuandaa lugha za kigeni zitakazoruhusiwa kufundishwa au kujifunza katika asasi

za elimu Tanzania. Lugha hizo, kwa maoni yangu, ni Kiingereza, Kifaransa, Kiarabu, lugha za

Uk. wa 17 kati ya 21

Mashariki ya Mbali (Kichina, Kijapani, Kirusi na Kikorea). Kila mwanafunzi (katika ngazi zote)

atatakiwa asome angalau somo moja la lugha ya kigeni;

c) Kuandaa mpango maalum wa jinsi ya kuwapata watu wafaao kuwa walimu, mfumo wao wa

mafunzo, pamoja motisha walimu wa masomo ya lugha ya Kiswahili na lugha za kigeni (ambazo

zitakuwa zinafundishwa kama masomo) ili kuboresha umilisi wa wanafunzi. Uboreshaji wa

ufundishaji wa lugha za kigeni uhusishe pia mataifa husika;

d) Kuandaa kamati zitakazojumuisha wataalamu wa tafsiri na ukalimani na wanazuoni wa fani

mbalimbali ili kuendeleza shughuli ya kutafsiri nyaraka za kufundishia na kujifunzia;

e) Kuanzisha programu za masomo ya tafsiri na ukalimani kama masomo ya lazima katika ngazi ya

elimu ya sekondari. Kisha kupanua Shahada za Tafsiri na Ukalimani katika Vyuo Vikuu

vitoavyo Shahada hizi, na;

f) Kuanza utekelezaji wa tamko la Uswahilishaji baada ya mwaka mmoja toka litakapoingizwa

katika katiba. Muda huo utatosha kwa hatua mbalimbali za maandalizi ya „mhamo huo wa

lugha‟ katika elimu, biashara (kubadilisha vitabu, matangazo, bidhaa n.k.).

5.0 Faida za Uswahilishaji

Iwapo Tanzania yote itawahilishwa, ni wazi kuwa itapata tija zifuatazo: Mosi, itaongeza ajira

kwa wananchi wake. Hivi sasa kuna Vyuo Vikuu kadhaa hapa nchini vifundishavyo masomo ya

Shahada za Lugha ya Kiswahili zifundishwazo kwa lugha ya Kiswahili (Shahada za Awali, za Umahiri

na za Uzamivu). Mifano yake ni Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Chuo

Kikuu cha Waislamu Morogoro. Baadhi ya mambo yafundishwayo katika programu hizo ni stadi za

uandishi, tafsiri, ukalimani, utafiti wa lugha, uhariri, na usomaji wa prufu. Wataalamu hawa ndiyo

rasilimali muhimu sana katika kuiswahilisha Tanzania kwani watahitajika sana katika „mhamo huu wa

lugha‟ kwa kushiriki katika michakato kama vile kuandika, kutafsiri, na kuhariri. Matumizi ya

wataalamu hawa hayataishia katika kipindi cha mhamo wa lugha tu, bali pia yatakuwa endelevu

Uk. wa 18 kati ya 21

kutokana na kuwa kuna bidhaa mbalimbali na wageni wengi waingiao nchini kila siku. Kwa kuwa nchi

itakuwa imeswahilishwa — Kiswahili kitakuwa kimetapakaa katika kila eneo, itawalazimu wageni hao

kuhitaji huduma za tafsiri na ukalimani kutoka kwa wenyeji. Hali hii ni tofauti na sasa ambapo hata

majina ya mitaa yameandikwa kwa Kiingereza. Vilevile, huduma muhimu, bidhaa na nyaraka

mbalimbali za kibinadamu zimewekwa kwa Kiingereza. Hali hii huwarahisishia kazi wageni wajao

nchini katika kujipatia huduma. Ajira pia zitaongezeka kwa Watanzania kuhitajika nje ya nchi — katika

mataifa yenye hamu ya kukitumia Kiswahili. Mataifa haya yapo mengi, na yanaendelea kuongezeka.

Nafasi hii ya kutoa huduma ya Kiswahili huko kwa hivi sasa, kwa kiasi kikubwa, imeshikwa na wa-

Kenya ambao, kitaaluma, wameimakinikia lugha ya Kiswahili kuliko Watanzania. Kwa upande

mwingine, hali hiyo ya kuongezeka kwa ajira za ndani na nje ya nchi, mbali na kuongeza pato la

Mtanzania mmojammoja, itakuwa inaongeza pato la taifa. Hivyo, kuongeza ustawi wa Tanzania kwa

ujumla.

Tija nyingine ni kuinua uelewa na uendeshaji wa mambo rasmi kama vile elimu, utabibu,

sayansi, sheria na teknolojia. Kwa kiasi kikubwa, mambo hayo hivi sasa huendeshwa kwa ugumu wa

kukariri na kulazimishwa. Hivyo, kwa namna moja au nyingine, kukwaza mnyiririko wa maendeleo.

Tija ya nne ni kuleta haki na usawa kwa Watanzania wote. Kama ilivyodokezwa hapo juu

mhamo wa kifikra wa Watanzania wengi kuhusu shule zifaazo kuwaelimisha watu wao, watu wasio na

uwezo ndiyo wawapelekao watoto wao katika shule za serikali. Wenye uwezo wengi hupeleka katika

shule zitumiazo lugha ya Kiingereza kama nyenzo ya mawasiliano na ya kufundishia. Wakiongozwa na

fikra za kuamini kuwa Kiingereza ni elimu, wamiliki wa shule hizi huweka mkazo zaidi katika kujua

lugha. Kwa upande wa kiasi cha maarifa, wahitimu wa shule hizi hawana tofauti yoyote na wahitimu wa

shule nyingine za serikali. Fikra za namna hiyohiyo zimewagubika pia waajiri wengi wa Tanzania

ambao wako tayari kumwajiri mtu tu kwa sababu ana uwezo wa kujieleza kwa Kiingereza hata kama

kimaarifa anazidiwa na yule asiye na uwezo wa kujieleza Kiingereza. Ni wazi kuwa, kwa mwenendo

huu, wahitimu wa shule za serikali huwa katika kundi la hasara zaidi kuliko wenzao wale waliohitimu

Uk. wa 19 kati ya 21

katika shule hizi „za Kiingereza‟. Hatimaye, kuweka upogo mkubwa wa ki-ajira baina ya Watanzania.

Hivyo, kama Tanzania itaiswahilishwa, ni wazi kuwa itasaidia hakuwakomboa wachochole ambao

wanaunda sehemu kubwa ya jamii.

6.0 Madhara ya Kutoswahilishwa kwa Tanzania kwa Kizazi cha Sasa na Baadaye

Iwapo nchi itaendelea kuwa katika hali hii ya kutoswahilishwa, Watanzania tutaendelea

kuzipoteza tija zilizobainishwa hapo juu. Yaani, jamii ya wanyonge wa kiuchumi wataendelea

kutengwa; tutaendelea kupoteza fursa ya ajira za ndani na nje kwa Watanzania wengi ambao wana sifa

ila wanakwamishwa na usomakinifu wetu katika Kiswahili. Vilevile, tutaendelea kuwa na kizazi butu

kielimu, kizazi cha kukariri au kama akiitavyo Kiputiputi (2007:107) kuwa ni kizazi cha unataji wa

kielimu; na siyo uchakataji wa kielimu. Kizazi cha kunata elimu ni kile ambacho kinaishi kwa kukariri

bila kuwa na uelewa wa dhati. Na kile cha uchakataji ni kinyume chake, yaani hupata elimu kwa uelewa

wa dhati na huwa na uwezo wa kuzalisha mawazo kutokana na elimu yao kwa uhuru na upevu. Kizazi

cha unataji ni hatari sana kwa ustawi wa taifa kwa sababu uwezo wake wa kutafiti, kuvumbua, na

kubuni ni mdogo sana. Tanzania, ambayo ina kiasi kikubwa sana cha kizazi cha unataji imo katika

hasara kubwa ya ki-ustawi. Hivyo, iwapo itaendelea kuwa katika hali hii ya kutoswahilishwa itazidi

kutumbukia katika giza la ustawi kutokana na kuendelea kudumaza uwezo wa kufikiri pamoja na

teknolojia asilia.

Madhara mengine ni kuporomoka kwa umoja wa kitaifa kutokana na kuwatenganisha

Watanzania kielimu, kiajira na kihadhi kama nilivyodokeza hapo juu. Matokeo yake huweza kuzaa

uwezekano mkubwa wa kuwapo kwa machafuko kutokana na fukuto la muda mrefu la manung‟uniko,

chuki na hasira za kitabaka.

7.0 Hitimisho na Mapendekezo: Kizazi cha sasa kifanye nini ili Kuiswahilisha Tanzania?

Shaaban Robert, ambaye ni miongoni mwa waasisi wa dhana ya kuiswahilisha nchi ya Tanzania, kupitia

kalamu yake, aliwahi kusema hivi:

Uk. wa 20 kati ya 21

“…wasio Waafrika wanadai kuwa Kiingereza kitumike… Waafrika wanadai kuwa

Kiswahili kitumike… katika kila pigano upande mmoja hushinda. Bila shaka,

Kiingereza kitashinda. Bali, yatabiriwa kuwa utakuwa ni ushindi wa kitambo tu…

Haiyumkiniki kuwa wenyeji wa mahali popote katika ulimwengu waweza kuridhika

kuishi katika lugha ngeni milele” (Shaaban Robert, 1948).

Kwa hakika, “kitambo” akisemacho Shaaban kimekwisha kupita sana! Kila kizazi kina dhima

yake ya msingi kinayopaswa kuitimiza. Vizazi vilivyotangulia vilihusika na majukumu mbalimbali

kama vile kutafuta uhuru, kutafuta nyenzo ya mawasiliano ya kitaifa, pamoja na kujenga misingi ya

umoja wa kitaifa. Nimedokeza hapo juu kuhusu hali ya kuulizana maswali yasiyo na majibu

inayoendelea hapa nchini kuhusu matumizi ya Kiingereza na Kiswahili. Nimedokeza pia kuhusu

kunung‟unikiana na kulaumiana kunakoendelea kuhusu ubutu wa kimaarifa na wa lugha ya Kiingereza

kwa wahitimu wa ngazi mbalimbali za elimu. Nimedokeza pia kuhusu kuwepo kwa kasi ya jongoo

katika ufikiwaji wa maendeleo hapa Tanzania. Bila shaka, dhima ya kizazi cha sasa ni kuondoa maswali

yasiyo na majibu, manung‟uniko pamoja na lawama kwa kushiriki kikamilifu katika hatua yoyote

itakayokuja mbele kuhusu kuishamirisha dhana ya Uswahilishaji. Haya, ili kujitofautisha na vizazi

vilivyopita, yanapaswa kufanywa kwa matendo siyo kuishia midomoni wala kuendelea kugugumia

mioyoni. Hii ndiyo mikakati ya kimatendo. Hivyo, ninapendekeza yafuatayo:

a) Kuanzia sasa, wananchi wa kawaida, wanafunzi wa ngazi zote, wafanyakazi na wengine wote

wenye mapenzi mema na nchi ya Tanzania tuhubiri kauli mbiu ya “Tuungane kwa Kiswahili

kwanza, mengine yatafuatia”;

b) Watanzania tuunganishe nguvu na kudai kuwapo na kutendeka kwa jambo hili. Miongoni mwa

mikakati iwezayo kukoleza nguvu ya tafiti zilizotangulia ni kulifanya suala hili kuwa ajenda ya

kitaifa. Aidha, kuhakikisha kuwa suala hili lijitokeze dhahiri katika katiba ya nchi; na

c) Kulifanya jambo hili liwe ndiyo dhima kuu ya kizazi cha sasa kwa taifa letu.

Uk. wa 21 kati ya 21

8.0 Bibliografia

Buliba, A. na Wenzake (2006). Isimujamii. The Jomo Kenyatta Foundation. Nairobi.

Gandhi, M.K. (1965). “Our Language Problem”. A.T. Hingorani (Mhar.). Bombay.

Kamugisha, N. R. (2010). “Implementation of Learner-Centered Approach and Materials in Field

Research for Improving Teaching and Learning of Geography in Advanced Level Secondary Education

in Tanzania: A Case of Morogoro Municipality”. Tasnifu ya Shahada ya Umahiri, Chuo Kikuu cha

Dodoma.

Mlama, P. na Matteru, M.L. (1978). “Haja ya Kutumia Kiswahili Kufundishia katika Elimu ya Juu”.

BAKITA.

Rubagumya, C.M. (Mhar.) (1989). Language in Education in Africa. Clevedon. Philadelphia,

Multilingual Matters Ltd.

Sikombe, Y.Y. (2010). “Lugha ya Kiswahili katika Kufundishi na Kujifunzia Elimu ya Juu”. Tasnifu ya

Shahada ya Umahiri katika Kiswahili. Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.

Simala, I. (2003). “Uzalendo wa Lugha ya Kiswahili katika Enzi ya Utandawazi” katika Kiswahili na

Utandawazi. BAKITA.

Tumbo-Masabo, Z.N. na E.F.K. Chiduo (2007). Kiswahili katika Elimu. Taasisi ya Uchunguzi wa

Kiswahili, Dar es Salaam.